Mawaziri wakuu wawili wa zamani
nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati watakutana katika duru ya pili ya
uchaguzi nchini humo baada ya kukosekana kwa mshindi wa moja kwa moja
wakati wa duru ya kwanza.
Mshindi hutakiwa kupata asilimia 50 ya kura zilizopigwa.Anicet Georges Dologuele, aliyeongoza alipata 24%, na atakutana na Faustin Touadera, aliyepata 19% ya kura, kwenye duru ya pili 31 Januari.
Bw Dologuele alikuwa waziri mkuu kati ya 1999 na 2001, na pia alihudumu kama waziri wa fedha nchini humo.
Bw Touadera alikuwa waziri mkuu katika serikali ya rais Francois Bozize, aliyepinduliwa 2013.
Watu zaidi ya milioni moja walishiriki uchaguzi huo mkuu wiki iliyopita, ambao ni wa kwanza tangu mapinduzi ya serikali ya Machi 2013.
Taifa hilo limegawanyika kwa misingi ya kidini.
Wagombea 20 kati ya 30 waliotaka kumrithi kaimu rais Catherine Samba-Panza walikuwa mapema wiki hii wamelalamikia udanganyifu uchaguzini na kutaka kura ziache kuhesabiwa na uchaguzi urudiwe.
Lakini wengi wao walishawishiwa baadaye na serikali ya mpito kuondoa malalamiko yao, na mahakama ya kikatiba inatarajiwa kuchunguza madai yao.
- Anicet Georges Dologuele 23.8% - 281,420
- Faustin Touadera 19.4% - 229,564
- Desire Kolingba 12.6% - 149,134
- Martin Ziguele - 10.8% - 121,009
Chanzo:Tume ya uchaguzi CAR
0 maoni:
Chapisha Maoni